Exodus 8

1 aNdipo Bwana akamwambia Musa, “Nenda kwa Farao ukamwambie, ‘Hili ndilo asemalo Bwana: Waachie watu wangu waende, ili wapate kuniabudu. 2 bKama ukikataa kuwaruhusu kuondoka, basi nitaipiga nchi yako yote kwa kuwaletea vyura. 3 cMto Naili utafurika vyura. Watakuja kwenye jumba lako la kifalme na katika chumba chako cha kulala na kitandani mwako, katika nyumba za maafisa wako na kwa watu wako, vyura hao wataingia katika meko yenu na kwenye vyombo vya kukandia unga. 4Vyura watapanda juu yako, juu ya watu wako na maafisa wako wote.’ ”

5 dNdipo Bwana akamwambia Musa, “Mwambie Haruni, ‘Nyoosha mkono wako ukiwa na ile fimbo yako juu ya vijito, mifereji na madimbwi, fanya vyura waje juu ya nchi ya Misri.’ ”

6 eNdipo Haruni akaunyoosha mkono wake juu ya maji ya Misri, nao vyura wakatokea na kuifunika nchi. 7 fLakini waganga wakafanya vivyo hivyo kwa siri ya uganga wao, nao pia wakafanya vyura kuja juu ya nchi ya Misri.

8 gNdipo Farao akamwita Musa na Haruni na kusema, “Mwombeni Bwana awaondoe vyura kutoka kwangu na kwa watu wangu, nami nitawaachia watu wenu waende kumtolea Bwana dhabihu.”

9 hMusa akamwambia Farao, “Ninakupa heshima ya kuamua ni wakati gani wa kukuombea wewe, maafisa wako na watu wako ili kwamba vyura watoke kwenu na kwenye nyumba zenu. Isipokuwa wale walio katika Mto Naili.”

10 iFarao akasema, “Kesho.”

Musa akamjibu, “Itakuwa kama unavyosema, ili upate kujua kwamba hakuna yeyote kama Bwana Mwenyezi Mungu wetu.
11Vyura wataondoka kwako na katika nyumba zako, kwa maafisa wako na kwa watu wako, ila watabakia katika Mto Naili tu.”

12Baada ya Musa na Haruni kuondoka kwa Farao, Musa akamlilia Bwana kuhusu vyura aliokuwa amewaleta kwa Farao. 13 jNaye Bwana akafanya lile Musa alilomwomba. Vyura wakafia ndani ya nyumba, viwanjani na mashambani. 14Wakayakusanya malundo, nchi nzima ikanuka. 15 kLakini Farao alipoona pametokea nafuu, akaushupaza moyo wake na hakuwasikiliza Musa na Haruni, kama vile Bwana alivyokuwa amesema.

Pigo La Tatu: Viroboto

16 lNdipo Bwana akamwambia Musa, “Mwambie Haruni, ‘Nyoosha fimbo yako uyapige mavumbi ya ardhi,’ nayo nchi yote ya Misri mavumbi yatakuwa viroboto.” 17 mWakafanya hivyo, Haruni aliponyoosha mkono wake wenye fimbo na kuyapiga mavumbi ya nchi, viroboto wakawajia watu na wanyama. Mavumbi yote katika nchi ya Misri yakawa viroboto. 18 nLakini waganga walipojaribu kutengeneza viroboto kwa siri ya uganga wao, hawakuweza. Nao viroboto walikuwa juu ya watu na wanyama.

19 oWaganga wale wakamwambia Farao, “Hiki ni kidole cha Mungu.” Lakini moyo wa Farao ukawa mgumu naye hakuwasikiliza, kama vile Bwana alivyosema.

Pigo La Nne: Mainzi

20 pKisha Bwana akamwambia Musa, “Amka mapema asubuhi na usimame mbele ya Farao wakati anapokwenda mtoni nawe umwambie, ‘Hili ndilo Bwana asemalo: Waachie watu wangu waende, ili wapate kuniabudu. 21Kama hutawaachia watu wangu waondoke nitakupelekea makundi ya mainzi juu yako, kwa maafisa wako, kwa watu wako na kwenye nyumba zenu. Nyumba za Wamisri zitajazwa mainzi, hata na ardhi yote ya Misri.

22 q“ ‘Lakini siku ile nitafanya kitu tofauti katika nchi ya Gosheni, ambapo watu wangu wanaishi, hapatakuwepo na makundi ya mainzi, ili mpate kujua kwamba Mimi, Bwana, niko katika nchi hii. 23 rNitaweka tofauti kati ya watu wangu na watu wenu. Ishara hii ya ajabu itatokea kesho.’ ”

24 sNaye Bwana akafanya hivyo. Makundi makubwa ya mainzi yalimiminika katika jumba la kifalme la Farao na katika nyumba za maafisa wake, pia nchi yote ya Misri ikaharibiwa na mainzi.

25 tNdipo Farao akamwita Musa na Haruni na kuwaambia, “Nendeni mkamtolee Mungu wenu dhabihu katika nchi hii.”

26 uLakini Musa akamwambia, “Hilo halitakuwa sawa. Dhabihu tutakazomtolea Bwana Mwenyezi Mungu wetu zitakuwa chukizo kwa Wamisri. Kama tukitoa dhabihu ambazo ni chukizo mbele yao, je, hawatatupiga mawe? 27 vNi lazima twende mwendo wa siku tatu mpaka tufike jangwani ili tumtolee Bwana Mwenyezi Mungu wetu dhabihu, kama alivyotuagiza.”

28 wFarao akamwambia, “Nitawaruhusu mwende kumtolea Bwana Mwenyezi Mungu wenu dhabihu huko jangwani, lakini hamna ruhusa kwenda mbali sana. Sasa mniombee.”

29 xMusa akajibu, “Mara tu nitakapoondoka, nitamwomba Bwana na kesho mainzi yataondoka kwa Farao, kwa maafisa wake na kwa watu wake. Hakikisha tu kwamba Farao hatatenda kwa udanganyifu tena kwa kutokuwaachia watu waende kumtolea Bwana dhabihu.”

30 yNdipo Musa akamwacha Farao na kumwomba Bwana, 31naye Bwana akafanya lile Musa alilomwomba. Mainzi yakaondoka kwa Farao, kwa maafisa wake na kwa watu wake, wala hakuna hata inzi aliyebakia. 32 zLakini wakati huu pia Farao akaushupaza moyo wake, wala hakuwaruhusu Waisraeli waondoke.
Copyright information for SwhKC